Rumah Musa ni mwanafunzi wa chuo kikuu kutoka Buram, Darfur Kusini, anayesoma katika Chuo Kikuu cha Red Sea huko Port Sudan. Kwa sasa anaishi katika nyumba za chuo kikuu. Rumah yuko mwaka wake wa mwisho wa chuo kikuu na alikuwa karibu kuhitimu na kurudi kwa familia yake huko Darfur. Hata kabla ya vita, hakuweza kutembelea familia yake kwa miaka miwili, na baada ya vita, hakuweza kuwasiliana na familia yake kutokana na kukatika kwa mtandao wa mawasiliano huko Darfur. Ametengana na familia yake kwa zaidi ya mwaka mmoja, na bado yuko Port Sudan. Kwa bahati nzuri, hatimaye aliweza kujua kuhusu familia yake kupitia marafiki, lakini ni vigumu kwa msichana wa umri wake kushindwa kuzungumza na wazazi wake kwa mwaka mzima.
Vita vilipozuka mjini Khartoum tarehe 15 Aprili 2023 viliwalazimu maelfu ya watu kukimbilia kusini mwa mji wa Wad Madani. Watu walifanya shule na mabweni ya chuo kikuu kama makazi ya muda. Baada ya hapo, mzozo huo kwa bahati mbaya pia ulienea hadi Wad Madani, ambako ilionekana kuwa kitovu cha shughuli za kibinadamu nchini Sudan.
Kutokana na idadi kubwa ya watu waliokimbia makazi yao huko Khartoum, baadhi walilazimika kuishi katika maeneo yasiyofaa kwa makazi ya binadamu. Picha hii ni ya shamba la kuku kaskazini mwa Madani limetelekezwa kwa zaidi ya miaka 15, limejaa nge na nyoka. Baada ya shule na nyumba za bweni kujaa watu waliokimbia makazi yao, takriban watu 1,200 waliokimbia makazi yao walilazimika kuishi katika shamba hili lililo katika eneo la pembezoni karibu na Mto Nile.
Khadija ni mmoja wa wahusika niliokutana nao katika shamba lililotelekezwa. Nilikuwa nafahamiana naye hapo awali wakati akiishi katika kitongoji cha Al-Azhari cha Khartoum. Ilikuwa hali ya kugusa moyo kukutana naye huko alipokuwa akijaribu kuokoa maisha yake. Ilikuwa wakati wa hisia na tulilia pamoja kabla sijampiga picha hii.
Kila mtu anayeijua Sudan anajua hadithi ya watoto wa Maiqoma, na ni mojawapo ya vituo muhimu sana vinavyohifadhi watoto wasio yatima. Kituo hicho huleta pamoja watoto wengi wachanga. Kituo cha Maiqoma kiko katika eneo la gereza, ambalo lilikuwa kwenye mstari wa moto wakati wa vita hivi. Kundi la wadau wamasuala ya kibinadamu, ikiwa ni pamoja na UNICEF na Mpango wa Chakula Duniani, WFP walishiriki katika kuwaondoa watoto hao kutoka Khartoum na kuwahamishia kwenye nyumba nyingine huko Madani. Picha hii ilikuwa wakati wanahamishiwa Madani. Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba vita hivyo vilisambaa hadi kwa raia na mashirika yalilazimika kuwahamisha sehemu mbalimbali na kuwasambaza miongoni mwa familia tofauti. Hadithi ya watoto hawa inatia uchungu.
Nilipiga picha hii wakati nikivuka kutoka mji wa Kosti nchini Sudan hadi mji wa mpaka wa Renk nchini Sudan Kusini. Eneo hili liko kwenye mpaka kati ya nchi hizo mbili, na ni eneo ambalo watu wanaishi kwa muda kabla ya kufika kwenye vituo vya usafiri ambapo mashirika ya kibinadamu yanapatikana kwa madhumuni ya kuwasajili. Upigaji wangu wa picha hii uliambatana na kuzorota kwa kiasi kikubwa kwa hali ya usalama huko Darfur na Kordofan, na idadi kubwa sana ya watu walikuwa wakiwasili - takriban watu 3,000 kwa siku - ambao wengi wao walikuja bila kitu au mali chache sana za kibinafsi. Hili ni moja wapo ya maeneo ambayo mtu huhisi kuchanganyikiwa sana.